HISTORIA YA MKOA KAGERA

 Ramani ya jumla ya mkoa kagera

General map


Detailed or descriptive map for kagera region 
Kagera, lilikuwa ni moja ya maeneo yaliyounda Jimbo lililoitwa “Lake Province”. Jimbo hili lilijumuisha Wilaya za Bukoba, Musoma, Shinyanga na Tabora. Baada ya uhuru mwaka 1962 mkoa ulibadilishwa jina na kuitwa ‘West Lake Region’ (Ziwa Magharibi) na kujumuisha Wilaya 4 za Ngara, Biharamuro, Karagwe na Bukoba. Jina hili (Ziwa Magharibi) lilidumu katika kipindi cha ukoloni na baada ya uhuru mwaka 1961 mpaka mwaka 1979 baada ya vita kati ya Tanzania na Uganda (Vita ya Kagera).


Mkoa ulipata jina la Kagera kutokana na Mto Kagera zamani ukijulikana kama “Akagera” ambao hutiririsha maji yake kutoka Rwanda kupitia Kaskazini na kumwaga maji yake katika ziwa Victoria


UKUBWA WA MKOA NA MAHALI ULIPO


Mkoa wa Kagera unapatikana Kaskazini Magharibi mwa nchi ya Tanzania. Makao Makuu ya Mkoa yapo katika mji wa Bukoba umbali wa kilometa 1500 kutoka Dar es Salaam, Mkoa huu unapakana na nchi ya Uganda kwa Kaskazini, Rwanda na Burundi kwa upande wa Magharibi,Mikoa ya Geita na Kigoma,  kwa upande wa Kusini. Pia Mkoa wa Kagera unapakana na  Ziwa Victoria kwa upande wa Mashariki ambapo kwa ndani ya Ziwa hilo mkoa unapakana na Mikoa ya Geita, Mwanza na Mara. Vile vile Mkoa wa Kagera uko Kusini mwa Ikweta kati ya Latitude 1 “00” na 2”45”. Mashariki mwa ‘Greenwich' katika Longitudi 30”25” na 32”40”


Mkoa wa Kagera una jumla ya eneo la Kilomita za mraba 35,686 kati ya hizo Kilomita za Mraba 25,513 ni eneo la nchi kavu ambalo ni sawa na asilimia 73 ya eneo lote la Mkoa na kilomita za mraba 10,173 ni eneo la maji sawa na asilimia 27. Mkoa una visiwa vikubwa katika Ziwa Victoria ambavyo ni Bumbire, Iroba, Kelebe, Goziba, Ikuuza na Mhutwe na visiwa vingine vidogo jumla vikiwa 27 vinavyokaliwa na watu na jumla ya visiwa 21 vidogo vidogo visivyokaliwa na watu.  Ukiacha mbali Wilaya ya Biharamulo ambayo ni tambarare, sehemu kubwa ya mkoa ni yenye milima na vilima vilivyogawanywa na mabonde yenye matingatinga. Upande wa magharibi wa mkoa mito mingi inamwaga maji yale katika Mto Kagera ambao nao humwaga maji yake katika Ziwa Victoria. 


Mwinuko wa nchi (altitude) ni kati ya mita 1,100 na 1,800 juu ya usawa wa Bahari. Mchanganuo wa kilomita za mraba kwa kila Halmashauri ni kama ifuatavyo: - Halmashauri ya Wilaya Biharamulo (5,627 km2), Halmashauri ya Wilaya Bukoba (5,071 km2), Bukoba Manispaa (80km2), Halmashauri ya Wilaya Karagwe (4,630 km2), Halmashauri ya Wilaya Kyerwa (3,086 km2), Halmashauri ya Wilaya Missenyi (2,709 km2), Halmashauri ya Wilaya Muleba (10,739 km2), na Halmashauri ya Wilaya Ngara (3,744 km2).


MUUNDO WA KIUTAWALA


Kiutawala Mkoa wa Kagera umegawanyika katika Wilaya Saba (7) ambazo ni Biharamulo, Bukoba, Karagwe, Kyerwa, Missenyi, Muleba na Ngara. Mkoa una Halmashauri za wilaya 7 na ya Manispaa moja (1), Tarafa 27, Kata 192, Vijiji vilivyosajiliwa 662, Mitaa 66 na Vitongoji 3,728. Aidha, Mkoa una Majimbo tisa (9) ya uchaguzi.


IDADI YA WATU


Mkoa wa Kagera una jumla ya watu 2,458,023 wanawake 1,252,340 na Wanaume 1,205,683 (sensa ya Mwaka 2012) Aidha, Pato la Mkoa wa Kagera ni Shilingi 1,760,458 ambapo pato la mwananchi mmoja mmoja ni Shilingi 716,209 (NBS Tanzania 2012) kwa mwaka.


WATU WA MKOA WA KAGERA


Kabla na baada ya kuja kwa wakoloni Mkoa wa Kagera ulikuwa na utawala wa Kimila (Chiefdoms) uliogawanyika katika himaya 8. Himaya hizo ni pamoja na Kyamutwara, Kihanja (Kanazi), Kiziba, Ihangiro, Bugabo, Karagwe, Biharamulo (Rusubi) na Maruku (Bukara).


Baadhi ya Watemi waliotawala himaya hizo ni pamoja na Emmanuel Rukamba (Kyamtwara), Rumanyika (Karagwe), Kasusura (Biharamulo), Lugomola (Bukara), Rutinwa (Kiziba), Kayo za (Bugabo), Kahigi (Kihanja) na Nyarubamba (Ihangiro). Kila mtemi alikuwa na walinzi wake walioitwa Warugaruga.


Makabila yanayopatikana hivi sasa katika mkoa wa Kagera ni pamoja na Wahaya ambao wanapatikana zaidi katika wilaya za Bukoba, Muleba na Missenyi. Makabila mengine ni Wanyambo, wanaopatikana katika Wilaya za Karagwe na Kyerwa, Wasubi katika wilaya ya Biharamulo, Wahangaza wanaopatikana katika Wilaya ya Ngara. Pia kuna Waha, Wazinza and Warongo.


Baada ya kuja kwa wazungu waliongeza ulimaji wa kahawa kama zao la biashara lililowasaidia kujiongezea kipato. Wakazi wa asili ya Kagera ni wabantu na wengi wao wanaasili ya Bunyoro. Wanaongea lugha sawa na ile ya Wanyoro, Wanyankole, Watoro na Wakiga. Busubi na Bugufi wana lugha na desturi sawa na Watusi, Wahutu na Waha. Lakini makabila hayo ni ya Wabantu wa Ziwa (Interlacustrine Bantu) na yanafanana mila na desturi.


Makundi hayo yaligawanyika katiya wachungaji (Bahima) ambao walitawala na wakulima (Bairu) ambao walitawaliwa na mara nyingi kudharauliwa. Bahima (Balangira) walikuwa na koo chache zipatazo 20 na walitawaliwa na Wahinda, Wabito na Wankango Bairu walikuwa na koo kama 130 zenye mashina 24 ambayo kiasili walikuwa Bairu lakini kwa kuoa katika Bahima au kufanya kazi kwa Watemi walipandishwa hadhi na kuwa Bahima (Batware). Kila ukoo uliitwa jina la Baba mwanzilishi wake na kina ukoo ulikuwa na kitu walichokatazwa kula (Omuziro) na mnyama walioshirikishwa nae (Ekyerumono).


HALI YA HEWA


Hali ya hewa ya Mkoa wa Kagera kwa ujumla ni ya joto la wastani wa 26.02 sentigredi. Mvua zinanyesha kwa wastani wa milimita 800-1,100 kwa mwaka kati ya mwezi Septemba na Januari na kati ya mwezi Machi na Mei. Mvua hizi ndizo zinazowezesha kuwepo kwauoto wa asili wa kuvutia katika maeneo mengi ya mkoa. Kwa miaka ya kawaida mkoa hupata mvua za uhakika za vuli na masika ambazo ni muhium kwa shughuli za kilimo na ufugaji.


SHUGHULI ZA KIUCHUMI


Uchumi wa wenyeji wa mkoa wa Kagera ulijikita katika mashamba ya migomba na kahawa. Chakula chao kikuu ni ndizi katika aina zake mbalimbali. Katika mashamba yao hulima mazao mengine kufuatana na msimu. Mazao hayo ni pamoja na maharage, mihogo, mahindi na mboga.



Msomi wetu

Tembelea bloggers yetu kwa ajili ya kupata habari mbalimbali za michezo burudani elimu nakadhalika

Post a Comment

Please Select Embedded Mode To Show The Comment System.*

Previous Post Next Post